Home » » MWAMKO WA WANAUME KUSHIRIKI KATIKA AFYA YA UZAZI

MWAMKO WA WANAUME KUSHIRIKI KATIKA AFYA YA UZAZI

Saa tano asubuhi katika kliniki ya Kirando iliyopo mkoani Rukwa, mama mmoja mjamzito anasubiri huduma katika ofisi ya mhudumu wa afya.
Amekuja kliniki kuangalia maendeleo ya ujauzito wake. Safari hii kaja peke yake lakini anasema siku za nyuma alishawahi kwenda hapo na mumewe.
Kwa kliniki ya Kirando kuwa na wanaume wanaowasindikiza wenza wao sio jambo geni, ndiyo maana hatua chache kutoka katika ofisi aliyomo mjamzito huyu, wanaume kadhaa wanaonekana wakichanganyika na wanawake waliokuja kliniki.
Wanaume hawa wengi wao wakiwa vijana, wamekuja kliniki kuwasindikiza wenza wao kujua maendeleo ya mimba na hata afya za
Inawezekana kwa baadhi ya watu ikawa kioja kusikia kuwa mume naye anakwenda kliniki sambamba na mkewe, lakini wanaume wengi wamebadili mtazamo kuhusu masuala yanayohusu afya ya uzazi.
Zamani iliaminika kwa wengi kuwa wajibu wa mwanaume ni kutungisha mimba, lakini kazi ya kuilea, kuzaa, afya na malezi ya mtoto ni majukumu ya mwanamke pekee.
Hata hivyo, kupitia elimu kwa umma na hamasa kwa jamii kupitia juhudi za Serikali na wadau wengine, ushiriki wa wanaume katika masuala ya afya ya uzazi umeongezeka.
Wanaume Rukwa
Mkoani Rukwa wanaume wengi wamebadilika kimtazamo na kitabia hasa baada ya wengi kufikiwa na mafunzo ya mradi wa ushiriki wa wanaume katika masuala ya afya ya uzazi (TMEP), unaofadhiliwa na Chama cha elimu ya afya ya uzazi cha Sweden (RFSU).
Meneja Mradi, Dk Cuthbert Maendaenda, anasema mradi pamoja na mengineyo unalenga kuhakikisha kuwa wanaume na wanawake wana haki sawa katika masuala ya uhusiano na uzazi.
‘’Ili uzazi utoke lazima wawili hawa washiriki pamoja lakini ikaonekana wajibu wa mwanaume unakwisha baada ya kusababisha mke kupata mimba, mengineyo kama kupima ujauzito, kumpeleka mtoto kliniki, kuzuia maambukizo ya mtoto kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto vinabaki kwa manamke,’’ anasema.
Anaongeza: ‘’Mradi wa TMEP unasisitiza wanaume kujua kuwa nao ni wateja wa masuala ya afya ya uzazi. Ili kuwepo na uhusiano mzuri tunataka wanaume wawasaidie wenza wao.’’

Mganga mfawidhi wa kituo cha afya Kirando, Dk Anastazi Kisinda anasema tangu jamii ifikiwe na mradi wa TMEP, ushiriki wa wanaume kuwasindikiza wenza wao kliniki kwa ajili ya kupata huduma za afya umekua kwa kiasi kikubwa.
“Siku za nyuma haikuonekana kama kitu cha kawaida, lakini sasa inaonekana kuwa kitu cha kawaida. Zamani hakuna mwanamume aliyekuja lakini sasa kwa siku hatuwezi kukosa wanaume 20 au 25 kutegemea ukubwa wa kliniki ya siku hiyo,’’ anaeleza.
Anasema ili kuhamasisha wanaume kuhudhuria kliniki, walianzisha utaratibu wa kuwapa kipaumbele wanawake wanaokuja na waume zao.
“ Awali changamoto tuliyoipata wanaume walifikiri kuja ni kupoteza muda, tukawapa ari wanawake waliokuja na wenza wao kwa kuwahudumia haraka kuliko wenzao, ‘’anasema.
Marieta Hamisi ni mwanamke aliyeamua kufunga kizazi. Anasema hakupata tabu kumshawishi mume wake haja ya kufanya hivyo baada ya kuwa na idadi ya kutosha ya watoto wanaoweza kuwahudumia.
“Nilipomweleza mume wangu hakunibishia, alinielewa hivyo tukafunga kizazi. Hapa kwetu wanaume wengi wanakwenda kliniki na wenza wao,’’ anasema Marieta ambaye ni mkazi wa kijiji cha Matai wilayani Kalambo.
Ukiondoa wanaume kwenda kliniki, mkazi wa Manispaa ya Sumbawanga, Joel Charanda, anasema haoni aibu kumsaidia katika majukumu ya nyumbani.
“Najua majukumu ya baba nikiwa nyumbani, nakwenda hata sokoni, nikirudi nabeba mtoto, wenzangu wananishangaa ukiangalia sisi bado ni vijana.Lazima nimsaidie mke wangu kwa sababu sijamuoa kuja kuwa mtumwa,’’ anasema.
Anaongeza: “Mwanaume hana budi kutambua kuwa yeye na mke wake wana majukumu sawa katika kuleta maendeleo.’’
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa