Home » » UTUMIKISHWAJI WATOTO SIKONGE WAPUNGUA

UTUMIKISHWAJI WATOTO SIKONGE WAPUNGUA




Mwandishi wetu, Sikonge-Tabora Yetu

Utumikishwaji watoto katika mashamba ya tumbaku na ufugaji wa ng’ombe katika jamii za Wasukuma na Wanyamwezi wilayani Sikonge Mkoani Tabora imepungua kutoka asilimia 90 hadi kufikia asilimia 50, baada ya elimu kutolewa kwa jamii.
            
Hayo yamesemwa na Bw. Ezekiel Basisi, mhamasishaji na mshauri wa Prosper kata ya Ipole, kwenye sherehe ya uelimishaji jamii kuondoa watoto katika utumikishwaji wa kilimo cha tumbaku iliyofanyika katika kijiji cha Udongo, kata ya Ipole wilayani Sikonge na kuhudhuriwa na wakazi wa vijiji vya Makazi na Mitwigu.

Aidha Bw, Basisi amesema licha ya kutoa elimu juu ya kuacha kutumikisha watoto katika jamii ya wafugaji, mashambani, majumbani na kazi zinginezo, pia mradi wa Prosper  umekuwa ukishirikiana na halmashauri ya wilaya Sikonge kutoa elimu ya mafunzo ya ujasiriamali kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15 na 17 na vikundi mbalimbali vya akina mama.

Meneja wa Prosper,  Bw, Christoher Luyenga, amebainisha kuwa mradi huo umefanikiwa kutoa mikopo kwa vikundi 10 vya wakinamama  wajasiriamali toka vijiji mbalimbali wenye thamani  ya sh. mil 43.5 kwa ajili ya kuendesha biashara ndogo ndogo ili kuwakwamua kutoka katika umaskini wa kipato.

Bw, Luyenga amesema kuwa mbali na kusaidia wajasiriamali, mradi huu pia umefadhili watoto wa shule za msingi wapatao 300 katika vijiji hivyo, ambapo vifaa mbalimbali vya shule na gharama nyinginezo zenye thamani ya sh milioni 15 vimetolewa kwa watoto hao na vinaendelea kutolewa mpaka watakapomaliza shule, lengo la madi huu ni kufadhili watoto wapatao 600.

Kwa upande wake Mratibu wa Prosper Wilayani Sikonge, Bi. Jesca Kibiki amesema lengo ni kuihamasisha jamii na kuijengea uwezo ili ipambane na ajira mbaya kwa watoto, ikiwa ni pamoja na kuihamasisha kulima zao hilo la tumbaku bila kutumikisha watoto.

Amesema mradi huo wa kupambana na utumikishwaji  watoto hapa mkoani Tabora, ni mradi wa miaka 4 na umefadhiriwa na taasisi ya kimataifa ya ECTL yenye makao makuu jijini Geneva, nchini Uswisi na umeanza mwezi Des.2011 na unatarajiwa kufungwa Des.2015.

Blogzamikoa

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa