Home » » BODI YAPENDEKEZA CHAMA KIVUNJWE

BODI YAPENDEKEZA CHAMA KIVUNJWE

Tabora. Bodi mpya ya Chama Kikuu cha Ushirika wa Wakulima wa Tumbaku Kanda ya Magharibi (Wetcu Ltd), imependekezwa kuvunjwa kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo ikiwamo kushindwa kulipa madeni ya wakulima.
Azimio la kuvunjwa kwa chama hicho kinaongozwa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)Mkoa wa Tabora, Hassan Wakasuvi, limetolewa na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC).
Katika kikao hicho wajumbe walionyeshwa kusikitishwa jinsi bodi hiyo yenye jukumu la kusimamia masilahi ya wakulima wa tumbaku, inavyoendelea kuwakandamiza.
Mbunge wa Sikonge, Said Nkumba alisema Wetcu Ltd inapaswa kulaumiwa kwa sababu imepewa jukumu la kuhakikisha matatizo yote yanayowakabili wakulima wa tumbaku na vyama vyao vya msingi yanatatuliwa, lakini hali imekuwa kinyume.
“Wetcu imeshindwa kabisa kuwasaidia wakulima, madeni yao ni makubwa hayajalipwa mpaka sasa kwa wilaya zote za Tabora. Hali hii inazidi kuwaongezea umaskini mkubwa tunatakiwa kuchukua hatua,” alisema Mkumba.
Alisema Wetcu imeshindwa kuweka mikakati endelevu na haina nia ya dhati kuondoa kero zinazomkabili mkulima, badala yake inamuongezea mzigo wa madeni.
Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe (CCM) alipongeza hatua ya Mkuu wa Mkoa huo, Fatma Mwassa kuleta timu ya wakaguzi kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) kufanya ukaguzi wa mapato na matumizi ya Wetcu.
“Mwenyekiti nakupongeza kwa kutuletea timu ya wakaguzi kutoka Ofisi ya CAG, naomba uchunguzi huo ufanyike haraka na watakaobainika kuhusika na wizi wa fedha za wakulima kupitia chama hicho wachukuliwe hatua kali,” alisema Tambwe.
Akizungumzia taarifa za uchunguzi wa zao hilo, Dk Phillips Mtiba ambaye ni Katibu Tawala Msaidizi (Uchumi), alisema kitendo cha wakulima wengi kutolipwa fedha zao kinawasababishia umaskini ambao hawakutarajia.
Naye Mkuu wa Mkoa huo, Fatma Mwassa alisema bodi ya Wetcu iliwekwa na Wizara ya Ushirika na Masoko kwa muda, hivyo ipo haja ya kufanya uchaguzi mpya kwa sbabu imeshindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo.
Aliongeza kuwa bodi hiyo imekuwa ikitoa zabuni kwa upendeleo, imeshindwa kulipa madeni ya wakulima hali ambayo inawaongezea ugumu wa maisha wakulima hao kwa kuwalimbikizia madeni, na kwamba kwa ujumla haiwatendei haki.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa