Home » » DK. MENGI KUTOA SH. MILIONI 10 KWA ATAKAYEFICHUA MUUAJI WA ALBINO

DK. MENGI KUTOA SH. MILIONI 10 KWA ATAKAYEFICHUA MUUAJI WA ALBINO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari makao makuu ya IPP jijini Dar es Salaam jana kuhusiana na kuvamiwa na kuuawa kwa Mapambano Mashili, mume wa mlemavu wa ngozi, Suzane Mungy, wakati akijaribu kumuokoa alipovamiwa na watu waliokuwa wakimkata mapanga katika kijiji cha Buhelele kata ya Nsimbo Wilaya ya Igunga mkoani Tabora juzi. IPP itatoa Sh. milioni 10 kwa atakayewezesha kukamatwa kwa waliotenda uhalifu huo na pia itawasomesha watoto wa marehemu. Kulia ni Gamario Mboya, kutoka shirika la Under The Same Sun (UTSS), na kushoto ni Katibu Mkuu wa Chama cha Walemavu wa Ngozi nchini, Ziada Nsemo. PICHA: KHALFAN SAID
Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, ameliomba Jeshi la Polisi mkoani Tabora kuhakikisha linawakamata na kuwafikisha mahakamani wote waliohusika na kukatwa kiwiko cha mkono mlemavu wa ngozi (albino), Suzan Mungi (35) na kutangaza dau la Sh. milioni 10 taslimu kwa mwananchi yeyote atakayetoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa watu hao.
Pia ameahidi kubeba jukumu la kuwasomesha watoto wawili wa Suzan, ambaye mumewe, Mapambo Mashili, aliuawa kikatili kwa kupigwa na kitu chenye ncha kali kifuani na kichwani wakati akijaribu kumnusuru mkewe (Suzan) asikatwe mkono wake na watu hao katika tukio hilo.

Katika tukio hilo, watoto hao wawili wameripotiwa pia kujeruhiwa na kulazwa hospitali.

Dk. Mengi alisema hayo alipokutana na viongozi wa Chama cha Albino Tanzania (TAS), ofisini kwake, jijini Dar es Salaam jana.

Alisema amefikia uamuzi huo kutokana na kuguswa na uchungu wa madhara yaliyowasibu albino na wengine, ambao wamekuwa ama wakikatwa viungo vya miili yao au kuuawa kabisa kwa sababu ya ulemavu wao.

“Ingekuwaje wewe ni mwanaume na Suzan ni mkeo, au ni mtoto wao, au mdogo wako au ni mtu wako wa karibu? Ungejisikiaje? Niwaachie Watanzania jibu la hilo swali. Tunachukua hatua gani kuwalinda watu hawa. Mtu hachagui, hakuzaliwa wala hakuomba kuwa mlemavu. Mungu hafanyi makosa katika kazi yake,” alisema Dk. Mengi.

Aliongeza: “Uongozi wa Jeshi la Polisi uchukue hatua za haraka hata ikibidi nyumba kwa nyumba wachukue hatua ili liwe fundisho kwa wengine na tuonyeshe kuwa tunawajali hawa wenzetu. Kama kuna mganga amehusika achukuliwe hatua.

Kama kuna mtu anatafuta madaraka achukuliewe hatua kali. Naliomba Jeshi la Polisi Tabora wahusika washikwe, wafikishwe mahakamani ili anayehusika aonje machungu. Aliyetumwa kukata mkono, mganga na kila aliyehusika wote washughulikiwe.”

Alisema yeye hana madaraka ya kuchukua, hivyo atatoa mchango wake kwa kumpa kiasi hicho cha fedha mwananchi yeyote atakayetoa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa wahusika na uhalifu huo, ikiwa ni pamoja na kuwasomesha watoto hao.

Naye Katibu Mkuu wa TAS, Ziada Nsemo, alimshukuru Dk. Mengi akisema ni mtu wa kwanza nchini kuguswa moyoni na kujitokeza hadharani kukemea vitendo vya ukatili vinavyofanywa dhidi ya albino.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa