Home » » WAZALISHAJI VYAKULA VYA WATOTO WAASWA

WAZALISHAJI VYAKULA VYA WATOTO WAASWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WIZARA ya Afya na Ustawi wa Jamii imewataka wajasiriamali kuzingatia mchanganyiko wa vyakula wanavyotumia kutengeneza unga wa lishe kwa watoto chini ya miaka mitano ili kuepuka athari za kiafya zinazoweza kujitokeza.

Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu Dar es Salaam jana Msemaji wa Wizara hiyo, Nsachris Mwamwaja alisema kuwa wajasiriamali wengi wamekuwa wakitengeneza unga huo bila kuzingatia mchanganyiko.

"Wajasiriamali na wazazi nyumbani wamekuwa wakitengeneza unga wa lishe kwa ajili ya watoto bila kuzingatia mchanganyiko wa makundi matano matano ya vyakula kitu ambacho kiafya ni hatari," alisema.

Mwamwaja alisema ni vema elimu inayotolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe (TFNC) ikazingatiwa kwani taasisi hiyo ina wataalamu wa kutosha na iko chini ya Wizara ya Afya.

Hivi karibuni katika maadhimisho ya Siku ya Unyonyeshaji maziwa ya mama,Daktari Bingwa wa Watoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Augustine Massawe alisema unga huo ni hatari kwa sababu mchanganyiko wake si mwafaka kwa watoto.

Dkt. Massawe alisema utengenezaji wa unga huo hauzingatii vipimo maalumu wala makundi ya virutubisho anavyopaswa kupata mtoto katika mlo mmoja, ambavyo ni wanga,protini,vitamini,mafuta na madini.

Alikosoa utengenezwaji wa unga unaochanganywa mahindi, mchele, ulezi, soya, mtama, karanga na dagaa.

"Mchanganyo kama hu haukubaliki kwa sababu katika mchanganyiko huu wa aina hii kuna orodha ya nafaka ambazo zina kirutubisho kimoja cha wanga na haziongezi virutubisho vingine",alisema.

Alipendekeza wazazi kutumia aina moja ya nafaka kama mahindi ambayo yanatoa wanga,mafuta na nyuzi.

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa