Home » » Wanawake wawili wauawa kinyama

Wanawake wawili wauawa kinyama

WANAWAKE wawili wilayani Nzega, mkoani Tabora, wameuawa kwa kukatwa katwa mapanga katika matukio mawili tofauti yaliyotokana na migogoro ya ardhi na kifamilia.
Tukio la kwanza limetokea katika Kijiji cha Iboja, Kata ya Sigili ambapo mwanamke mmoja ameuawa kwa kukatwa mapanga kutokana na ugomvi wa mashamba.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Diwani wa kata hiyo, Pelle Izengo, alimtaja mwanamke huyo kuwa ni G’wallu Kibunga (55), mkazi wa kijiji hicho.
Alisema tukio hilo limetokea Septemba 7, mwaka huu, majira ya saa tatu usiku, ambapo wauaji hao ambao hadi sasa hawajajulikana waliingia ndani ya nyumba ya mwanamke huyo na kuanza kumshambulia kwa mapanga na kusababisha kifo chake.
Pelle alisema sababu ya mauaji hayo ni ugomvi wa mashamba ambapo mwanamke huyo alishinda kesi yake katika Mahakama ya Ardhi Tabora.
Diwani huyo aliwataka wananchi wa kata hiyo kutojichukulia sheria mikononi, badala yake wafuate sheria ili kunusuru mauaji ya aina hiyo.
Katika tukio la pili, mwanamke aliyefahamika kwa jina la Kundi Msweya (70), mkazi wa Kijiji cha Mbagwa, ameuawa kwa kukatwa mapanga na watu wasiofahamika kijijini hapo.
Tukio hilo limetokea Septemba 4, mwaka huu, majira ya saa tano usiku ambapo watu hao walimvamia ndani na kuanza kumshambulia kwa mapanga hadi kusababisha kifo chake.
Matukio hayo yamethibitishwa na Jeshi la Polisi huku upelelezi ukiendelea ili kubaini waliohusika na mauaji hayo.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa