Home » » WALIOFARIKI, KUJERUHIWA AJALI YA TABORA WATAJWA

WALIOFARIKI, KUJERUHIWA AJALI YA TABORA WATAJWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 

MAJINA ya abiria waliofariki na kujeruhiwa katika ajali mbaya iliyohusisha mabasi mawili ya AM Coach namba T 803 AGN aina ya Scania na Sabena namba T 110 ARV aina ya Scania, katika Kijiji cha Mlogola, Wilaya ya Sikonge, mkoani Tabora yametambuliwa.

Katika ajali hiyo ambayo imetokea Agosti 19 mwaka huu, basi la AM lilikuwa likitokea jijini Mwanza kwenda Mpanda na Sabena likitokea mkoani Mbeya kwenda Tabora ambayo yaligongana uso kwa uso na kusababisha vifo vya watu 16, majeruhi 81.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Suzani Kaganda alisema kati ya abiria 16 waliofariki, maiti za watu 13 zimetambuliwa na ndugu zao lakini miili ya abiria watatu bado haijatambuliwa na imehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa Kitete.

Aliwataja waliokufa kuwa ni Patrick Fumbuka, mkazi wa Mbeya, Fred Alex, Emmanuel Madochi Senga na Mabaga Benedicto Peter waliokuwa wanatokea mkoani Mbeya.

Wengine ni Nicholaus James, mkazi wa Geita, Aristideth Shirima ambaye ni dereva wa basi la AM na James Komba ambaye ni dereva wa basi la Sabena aliyekatwa kichwa na bati.

Wengine ni Jackline Gregin Lumendika, Nasma Zenda mwenye umri kati ya miaka 6-7, na mtoto mdogo wa kiume anayekadiriwa kuwa na umri wa mwaka mmoja.

Waliofariki katika ajali hiyo, 10 ni wanaume, wanawake wanne pamoja na watoto wawili mmoja wa kiume, mwingine ni wa kike ambapo chanzo cha ajali ni mwendo kasi.

Kamanda Kaganda alisema katika basi la Sabena kulikuwa na wanafunzi waliokuwa wanakwenda kufanya mitihani katika Chuo cha Kilimo Tumbi, kilichopo mkoani humo wakitokea Mikoa ya Mbeya na Iringa ambao ni Anna Kalimo kutoka Iringa na Joyce Mgeni kutoka Mbeya.

Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Sikonge, John Buswelu, alisema majeruhi 63 wameruhusiwa na wengine watatu hali zao bado mbaya na wamepelekwa Hospitali ya Mkoa kwa matibabu zaidi.

"Majeruhi wengi walioruhusiwa walikuwa na majeraha madogo madogo na michubuko katika maeneo mbalimbali ya miili yao, wanaendelea kutumia dawa wakiwa nyumbani kwao," alisema.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa, Deus Kitapondya, alisema hadi jana walikuwa wamepokea majeruhi 18 ambao walishindikana kutibiwa katika Hospitali ya Sikonge.

Majeruhi hao ni Meena Shilindye, Silvesta John, Nyorobi Masaga, Salum Hamisi, Athumani Jafari, Samweli Asubisye, Mgeta aliyekuwa akienda mkoani Mwanza, Josephat Weya, Paulo Nyanda, Amosi Dominick, Sgt. Joseph Msumari na Scola Kadati.

Wengine ni Jenifa Sanga, Tora Mbilinyi, Sikujua Saimon na mtoto mdogo mwenye umri wa mwaka moja ambaye mzazi wake wamefariki katika ajali hiyo pamoja na majeruhi ambaye hawezi kuzungumza na jina lake halijaweza kufahamika mara moja.

Aliongeza kuwa, jeshi hilo linaendelea na uchunguzi wa ajali hiyo na ukikamilika, wote ambao watabainika kuwa na makosa watafikishwa mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.

Alitoa pole kwa familia ambazo zimewapoteza ndugu zao kwenyeajali hiyo na kuwaombea majeruhi wote wapone haraka.

Salamu za JK kwa RC

Katika hatua nyingine, Rais Jakaya Kikwete, amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa huo, Bi. Fatma Mwasa kutokana na ajali hiyo akisema ameshtushwa, kusikitishwa na ajali hiyo ambayo imegharimu maisha ya watu na kujeruhi wengine.

"Pokea salamu zangu za rambirambi kutokana na ajali hii, kupitia kwako, naomba unifikishie salamu za rambirambi na pole kwa wafiwa wote kwa kupotelewa ghafla na wapendwa wao..namuomba Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema azipokee na kuzilaza roho za marehemu wote mahala pema peponi," alisema Rais Kikwete.

Rais Kikwete amewaomba wafiwa wote wawe na moyo wa uvumilivu na ujasiri wakati huu ambao ni mgumu sana kwao wanapoomboleza vifo vya ndugu na jamaa zao.

Alisisitiza umakini na usimamizi mzuri wa Sheria za Usalama Barabarani kutoka kwa mamlaka zinazohusika ili maisha ya wananchi wasio na hatia yasiendelee kupotea na kusababisha simanzi kwa familia, kupotea kwa nguvukazi muhimu ya Taifa.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa