Home » » CCM Tabora hali si shwari

CCM Tabora hali si shwari

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


ZAIDI ya wanachama 130 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika Manispaa ya Tabora, wamefunga ofisi ya Katibu wa chama hicho Wilaya ya Tabora Mjini, Bw. Bakari Lwasa na kuandamana hadi Ofisi ya CCM Mkoa ili kushinikiza aondolewe mara moja.

Wakiwa katika Ofisi ya CCM mkoani humo, wanachama hao walimkuta katibu wa chama hicho mkoani humo, Bi. Janeth Kayanda, wakiwa na mabango yaliyokuwa yakimtuhumu Bw. Lwasa kwa makosa ya ufujaji wa sh. milioni nane.

Baadhi ya mabango hayo yalisema; "Bakari hatukutaki, nenda kwenu Kaliua, umekuja kuua chama, umeharibu chama chetu".

Akizungumza kwa niaba ya wanachama wenzake, Bw. Deus Malugu alisema Bw. Lwasa amekigawa chama hicho kwa muda mrefu, kushiriki njama za kuwachafua baadhi ya viongozi na kushiriki kukikosesha ushindi CCM katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji mwaka 2014.

Alisema Katibu huyo ameshiriki katika upotevu wa sh. milioni nane za chama, Kata ya Gongoni na kuanzisha matawi mawili ya CCM ambayo ni Mdoe na Bachu bila kuwashirikisha wenzake jambo ambalo ni tabia ya ubinafsi.

Tuhuma nyingine zilizotolewa dhidi ya Bw. Lwasa ni kugawa sh.50,000 kwa Makatibu Kata wawili (majina yanahifadhiwa), ili wawe mashahidi dhidi ya Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM Taifa, Emmanuel Mwakasaka anayedaiwa kuanza kampeni ya
kutaka ubunge wa Jimbo la Tabora Mjini kabla ya muda.

Bw. Malugu alisema mgogoro baina yao na Bw. Lwasa upo muda mrefu ambapo Mwenyekiti wa CCM mkoani humo ambaye amemaliza muda wake, Hassan Wakasuvi na Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Bw. Abdulrahman Kinana, waliahidi kuupatia
ufumbuzi lakini hadi sasa wapo kimya.

Kwa upande wake, Bw. Lwasa alipoulizwa juu ya tuhuma hizo, alisema yeye hajui lolote na hafahamu kama wanachama hawamtaki au kuna maandamano ya kumkataa.

"Mimi sijui kama hawanitaki, sijui kama kuna wajumbe ambao wameandamana kwenda Ofisi ya Katibu wa CCM Mkoa kunikataa na sina taarifa kama ofisi yangu imefungwa," alisema.

Baada ya kupokea maandamano ya wanachama hao, Kayanda alipokea taarifa yao na kuahidi kuyafanyia kazi malalamiko yao kwa kuyafikisha katika uongozi wa CCM Taifa kwa hatua zaidi.

Alisema CCM Mkoa itampa Bw. Lwasa ofisi ya muda wakati wakisubiri uamuzi wa mwisho kutoka kwa uongozi wa juu

 Chanzo Gazeti la Majira 



 


 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa