Home » » KUWAIT YAIPATIA TANZANIA MKOPO NAFUU WA UJENZI WA BARABARA MKOANI TABORA

KUWAIT YAIPATIA TANZANIA MKOPO NAFUU WA UJENZI WA BARABARA MKOANI TABORA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Na Benny Mwaipaja, WFM, Dar es salaam
Serikali ya Kuwait imeahidi kuipatia Tanzania mkopo wenye masharti nafuu wa dola za Kimarekani milioni 34 sawa na zaidi ya shilingi Bilioni 74.8 kwa ajili ya ujenzi wa barabara yenye urefu wa Kilometa 85 kwa kiwango cha lami kutoka eneo la Chaya hadi Nyahua mkoani Tabora.
Ahadi hiyo imetolewa Jijini Dar es salaam na mwakilishi wa Balozi wa Kuwait hapa nchini, Bw. Mohammad Rashid Alamiri, aliyeongoza ujumbe kutoka Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait, ulipomtembelea na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ambapo wamejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kiuchumi na kijamii kati ya Tanzania na Kuwait.
Dkt. Mpango ameushukuru Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait (Kuwait Fund) kwa kuipatia Tanzania mkopo  huo wenye masharti nafuu utakaochochea maendeleo kwa Watanzania hususani wanaoishi katika maeneo ambayo barabara itajengwa kwa kuwa watarahisishiwa usafiri na usafirishaji wa bidhaa zao hivyo kukuza uchumi wao binafsi na Taifa kwa ujumla.
Amesema kuwa kipande hicho cha barabara kutoka Chaya hadi Nyahua, ambacho kiko Barabara Kuu itokayo Dar es salaam kwenda katika mikoa ya Tabora na Kigoma, licha ya umuhimu wake katika kukuza biashara na usafiri na usafirishaji wa abiria na mizigo ikiwemo inayokwenda nchi jirani, ilikuwa haijapata fedha kwa ajili ya ujenzi wake.
“Riba waliyoiweka mezani kwa mazungumzo ni asilimia 2 lakini nimewaomba waangalie uwezekano wa kuiteremsha walau ifike asilimia 1.5 na wamependekeza kipindi cha kuanza kulipa mkopo kiwe miaka ishirini ijayo lakini nimewaomba wasogeze hadi kufikia miaka 25 kama ilivyo kwa mradi wa Hospitali ya Mnazimmoja” aliongeza Dkt. Mpango
Dkt. Mpango amesema Serikali ya Kuwait kupitia Mfuko wake huo wa Maendeleo wameonesha nia ya kutoa mkopo wenye masharti nafuu kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa Hospitali ya Mnazi Mmoja iliyoko Visiwani Zanzibar.
“Nawahakikishia kuwa baada ya muda si mrefu wananchi wa mikoa ya Tabora na Kigoma watarajie kuona mkandarasi akiingia kazini ili kujenga barabara hii muhimu sana kwao na kwa uchumi wa Taifa kwa ujumla” Alisisitiza Dkt. Mpango.
Ameeleza kuwa ujenzi wa kipande cha barabara hiyo kutoka Chaya hadi Nyahua  unatarajia kugharimu shilingi Bilioni 61 lakini Kuwait haitatoa fedha zote hivyo ameuomba Mfuko huo uangalie uwezekano wa kutoa kiasi hicho chote cha fedha  ili uweze kukamilika mapema.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa