Home » » Askari 9 JKT watuhumiwa kuua mwananchi

Askari 9 JKT watuhumiwa kuua mwananchi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


MKAZI wa Kata ya Chemchem katika Manispaa ya Tabora, Asha Kayamba amemuonba Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP) na vyombo vya ulinzi na usalama vimsaidie ili askari wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) waliompiga mwanawe na kumsababishia kifo wachukuliwe hatua za kisheria.
Katika barua yake, amemlalamikia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuwaachilia askari tisa wa Kikosi cha 823 JKT Msange kwa madai ya kukosekana ushahidi.
Asha katika barua hiyo ya Desemba 19, 2015, alisema anasikitika kuona haki yake inapokonywa na kauli ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwamba kijana wake Omary Zuberi Shaban (19) ambaye sasa ni marehemu, aliuawa na wananchi wenye hasira.
“Kwa kweli nilipatwa na mshtuko mkubwa sana baada ya kuona haki yangu inapokonywa kwa kisingizio cha mtoto wangu kuuawa na watu wenye hasira,” alieleza Asha katika barua yake kwa DPP.
Alibainisha kuwa mwanawe alishambuliwa na wanajeshi hao (majina na vyeo vyao tunayahifadhi) mchana na wala wananchi hawakuhusika katika tukio hilo kwani wao walikuwa ni watazamaji tu.
Alisema mwanaye alipigwa na askari hao Septemba 10, mwaka jana na alilazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kitete kwa siku nne hadi alipoaga dunia Septemba 13, 2016 saa tano usiku.
Barua hiyo ilieleza kuwa Polisi ilifanya upelelezi wa tukio hilo na kuwatia nguvuni watuhumiwa tisa wakati mama wa marehemu, Regina Masuva, kijana aliyenusurika Zuberi Haruna, Mwaka Zuberi (mama mzazi wa Zuberi) na watu wengine walitoa maelezo kuhusu tukio hilo.
Alifafanua kuwa Septemba 20, 2016 watuhumiwa wa mauaji ya mwanawe ambao ni askari tisa wa Kikosi cha 823 Msange JKT walifikishwa mahakamani na kusomewa mashtaka na Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Samson Kabigi mbele ya Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Agatha Chugulu.
“Baada ya kusomewa mashitaka hayo, kesi hiyo ilipangwa kutajwa Oktoba 13, 2016 na Oktoba 28, 2016. Lakini siku hiyo watuhumiwa hao hawakufikishwa mahakamani.
“Nilipohoji kwa nini nilijibiwa kuwa walifanya fujo ndani ya mahabusu ya gereza la Uyui mjini Tabora, jambo lililowafanya wapewe adhabu hivyo hawataweza kufika,” alieleza mama huyo katika barua hiyo.
Alisema shauri hilo lilipangwa kutajwa Novemba 10, mwaka huu, nilipofika siku hiyo watuhumiwa walikuwepo mahakamani ambapo kesi yao ilipangwa kutajwa tena tarehe 24 Novemba, mwaka huu.
Alisema kuwa utata ndio ulianzia hapo.
Alidai kuwa kabla ya kufika tarehe hiyo, watuhumiwa wote tisa walionekana mtaani jambo ambalo lilimpa mshituko mkubwa na kufanya afuatilie mahakamani, Polisi na Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali mjini Tabora bila kupata majibu muafaka.
Alidai alipofika Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali, alikutana na ofisa aliyemtaja kwa majina ya Jackson Bulashi ambaye alidai kuwa alimjibu kwamba watuhumiwa hao waliokuwa wanakabiliwa na shauri la mauaji, wameachiwa kwa kuwa hakuna ushahidi wa kujitosheleza.
 CHANZO GAZETI LA HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa