Home » » MADIWANI WACHOCHEZI KUTUMBULIWA

MADIWANI WACHOCHEZI KUTUMBULIWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Lucas Raphael, Igunga
Mwanasheria wa Serikali Mkoa wa Tabora, Richard Lugomela
SERIKALI imesema haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria madiwani, watakaobainika kuleta uvunjifu wa amani katika kata zao na halmashauri kwa ujumla.
Kauli hiyo imetolewa na Mwanasheria wa Serikali Mkoa wa Tabora, Richard Lugomela (pichani) kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika mjinji hapa. Lugomela alisema madiwani wa Igunga wameshindwa kutatua kero zinazowakabili wananchi waliowachagua na badala yake wameamua kuendeleza migogoro ya kutokuelewana wao kwa wao huku wakijua kufanya hivyo ni makosa kisheria.
Alisema serikali Mkoa wa Tabora pamoja na wilaya zake, wamejipanga kikamilifu kuhakikisha wananchi wake pamoja na mali zao wanaishi kwa amani na usalama pasipo kuingiziwa migogoro na madiwani wao. Alibainisha kuwa diwani atakayebainika kuweka makundi ya kukwamisha juhudi za serikali za kuwatumikia wananchi na kuendelea kuleta uvunjifu wa amani, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake na kuwataka madiwani kuacha kuleta migogoro ya kufarakana kwa maslahi binafsi.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Igunga, Godslove Kawishe akizungumza kwa niaba ya mkuu wa wilaya, John Mwaipopo, aliwataka madiwani kwa kushirikiana na wenyeviti wa vitongoji na vijiji pamoja na watendaji wa vijiji kata kutatua kero za wananchi kwa wakati.
Aliwaagiza viongozi hao kusimamia kilimo pindi mvua zitakapoanza kunyesha, ambapo kila kaya inatakiwa kulima hekari moja ya zao la chakula ili kukabiliana na janga la njaa. Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Igunga, Revocatus Kuuli alisema migogoro ya madiwani waliyonayo, yeye na watumishi wenzake haiwahusu, kwani wao wanaendelea kufanya kazi kwa ushirikiano na ndiyo maana mapato ya halmashauri yanaendelea kupanda hadi sasa.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa