Imeandikwa na Lucas Raphael, Igunga
Mwanasheria wa Serikali Mkoa wa Tabora, Richard Lugomela
 
  SERIKALI imesema haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria 
madiwani, watakaobainika kuleta uvunjifu wa amani katika kata zao na 
halmashauri kwa ujumla.
 
Kauli hiyo imetolewa na Mwanasheria wa Serikali Mkoa wa Tabora, 
Richard Lugomela (pichani) kwenye kikao cha baraza la madiwani 
kilichofanyika mjinji hapa. Lugomela alisema madiwani wa Igunga 
wameshindwa kutatua kero zinazowakabili wananchi waliowachagua na badala
 yake wameamua kuendeleza migogoro ya kutokuelewana wao kwa wao huku 
wakijua kufanya hivyo ni makosa kisheria.
Alisema serikali Mkoa wa Tabora pamoja na wilaya zake, wamejipanga 
kikamilifu kuhakikisha wananchi wake pamoja na mali zao wanaishi kwa 
amani na usalama pasipo kuingiziwa migogoro na madiwani wao. Alibainisha
 kuwa diwani atakayebainika kuweka makundi ya kukwamisha juhudi za 
serikali za kuwatumikia wananchi na kuendelea kuleta uvunjifu wa amani, 
hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake na kuwataka madiwani 
kuacha kuleta migogoro ya kufarakana kwa maslahi binafsi.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Igunga, Godslove Kawishe akizungumza kwa 
niaba ya mkuu wa wilaya, John Mwaipopo, aliwataka madiwani kwa 
kushirikiana na wenyeviti wa vitongoji na vijiji pamoja na watendaji wa 
vijiji kata kutatua kero za wananchi kwa wakati.
Aliwaagiza viongozi hao kusimamia kilimo pindi mvua zitakapoanza 
kunyesha, ambapo kila kaya inatakiwa kulima hekari moja ya zao la 
chakula ili kukabiliana na janga la njaa. Mkurugenzi Mtendaji wa 
Halmashauri ya Wilaya ya Igunga, Revocatus Kuuli alisema migogoro ya 
madiwani waliyonayo, yeye na watumishi wenzake haiwahusu, kwani wao 
wanaendelea kufanya kazi kwa ushirikiano na ndiyo maana mapato ya 
halmashauri yanaendelea kupanda hadi sasa.
CHANZO HABARI LEO 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment