Imeandikwa na Lucas Raphael, Igunga
KIJANA muuza dawa za binadamu anayeishi Kijiji cha Mazira Kata ya 
Goweko, Igunga,Tabora, Shamsi Almasi (26) anashikiliwa na Polisi kwa 
tuhuma ya kusababisha kifo cha kichanga cha siku moja cha kike.
 
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Grayston Mushi alithibitisha tukio 
hilo kutokea Novemba 8, mwaka huu saa 9 alasiri Kijiji cha Mazira, Kata 
ya Goweko. Alisema Maria Andrea, mjamzito anayeishi Kijiji cha Buhekela 
alipopatwa na uchungu alienda kwa huyo kijana Almasi kuzalishwa lakini 
bahati mbaya mtoto alitanguliza miguu kichwa kikabaki. Alisema kijana 
huyo baada ya kuona ameshindwa kumzalisha mama huyo mjamzito, aliamua 
kunyofoa kiwiliwili cha kichanga hicho na kuacha kichwa tumboni mwa 
mama.
Hata hivyo, alipoona hali hiyo alimwambia mume wa Maria, John 
Isanzule (37) ampeleke Hospitali ya Ndala kwa matibabu zaidi huku mama 
huyo akiwa hana fahamu. Aidha, Kamanda Mushi alisema baada ya kukamatwa 
na kuhojiwa na Polisi, iligundulika kijana huyo hana taaluma ya udaktari
 au ukunga wala uuguzi na upelelezi ukikamilika atafikishwa mahakamani.
Akizungumza kwa shida akiwa amelazwa wodi ya wazazi Hospitali ya 
Misheni ya Ndala, Maria alisema kijana aliyemzalisha alishindwa ndio 
maana alinyofoa kiwiliwili cha kichanga na kuacha kichwa. Kaimu Mganga 
Mkuu wa Hospitali ya Misheni Ndala, George Mgalega amekiri kumpokea 
Maria akiwa hajitambui. “Ni kweli tulimpokea akiwa hajitambui na 
tulimfanyia upasuaji na kufanikiwa kutoa kichwa cha kichanga na hali 
yake inaendelea vizuri baada ya kupatiwa huduma zote zinazostahiki,” 
alieleza.
CHANZO HABARI LEO 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment