Home » » Madiwani Sikonge wataka kukamilishwa Vituo vya Afya

Madiwani Sikonge wataka kukamilishwa Vituo vya Afya

MADIWANI katika halmashauri ya wilaya ya Sikonge wametaka kukamilishwa ujenzi wa vituo vya Afya unaosuasua katika baadhi ya Kata.

Hayo yamebainishwa katika kikao maalumu cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kilichoketi  kwa ajili ya kupitisha bajeti ya maendeleo kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015.

Diwani wa kata ya Tutuo, Mh.Rashid Magope amesema anasikitishwa na ujenzi wa kituo cha Afya Tutuo kutokamilika wakati fedha ilishatengwa na akaomba halmashauri  ikamilishe haraka ujenzi wake kwani wananchi wake wanahangaika sana kutafuta huduma za Afya.

Naye diwani wa kata ya Kipili, Mh.Hamid Manzi ameomba halmashauri hiyo ifanye kila iwezalo ili ujenzi wa kituo cha afya Kipili ukamilike haraka kwa kuwa kituo hicho ni mkombozi pekee kwa wananchi wake kwani wanalazimika kutembea umbali mrefu sana kutafuta huduma za afya.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Shadrack Mhagama akifafanua hoja za madiwani hao amesema halmashauri yake imetenga fedha za kutosha kushughulikia mapungufu mbalimbali yanayovikabili vituo vya afya ikiwemo hospitali ya Mazinge na kituo cha afya Tutuo.

Amesema kero zinazokikabili kituo cha afya Kipili zinafahamika hivyo akabainisha kuwa wamejipanga kuzifanyia kazi katika bajeti ya mwaka wa fedha ujao 2015/2016 kwa sababu kero za namna hiyo ni nyingi hawawezi kuzitatua zote kwa bajeti ya mwaka huu wa fedha.

Aidha amebainisha kuwa katika bajeti ya mwaka  2014/2015 wameweka kipaumbele cha kutatua kero katika hospitali ya Mazinge,zahanati ya Mwenge iliyoko katika kata ya Kitunda na  Mwamayunga iliyoko katika kata ya Kisanga.  

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa