Home » » Wachimbaji wadogo waomba eneo la mgodi

Wachimbaji wadogo waomba eneo la mgodi

WACHIMBAJI wadogo wa dhahabu katika machimbo madogo ya Mwanshina katika Kijiji cha Nhobola wilayani Nzega mkoani Tabora, wameiomba serikali kuwapatia kibali cha kuchimba dhahabu pembezoni mwa mgodi mkubwa wa Resolute ili wakidhi mahitaji yao.
Wakizungumza katika mkutano wa kijiji mbele ya Mkuu wa Wilaya (DC) ya Nzega, Bituni Msangi, walisema kuwa serikali kupitia Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo awape kibali cha kuendesha shughuli zao kutokana na mwekezaji wa mgodi huo kukamilisha shughuli za uchimbaji mwaka 2015.
Mwenyekiti wa wachimbaji hao, Joseph Mabondo alisema kuwa mgogoro uliopo kati yao na serikali ni kutokana na kukosa eneo la kuchimba dhahabu huku wawekezaji wakiwa na eneo kubwa wasilotumia.
Joseph aliiomba serikali kusikiliza kilio hicho ili waweze kupatiwa kibali cha kuchimba dhahabu kwa uhuru kama ilivyo katika baadhi ya sehemu nyingine.
Alisema kuwa kitendo cha kuwapiga marufuku na kuwafukuza katika machimbo hayo kinajenga mahusiano mabaya kati yao na serikali wakati wana haki ya kupewa nafasi ya kuchimba ili kukidhi mahitaji yao na kukuza uchumi.
“Tunamuomba waziri husika na naibu wake Maselle watusaidie suala hili ili tuweze kujikwamua kimaisha kwani mambo ya kukimbizana na kufukuzana sio mazuri, inapaswa kutuangalia kwa macho mawili ili nasi tunufaike na rasilimali zetu,’’ alisema.
Alisema kuwa kwa sasa kuna baadhi ya wawekezaji wanamiliki maeneo makubwa na kuyatumia katika shughuli zao za uchimbaji wakati wachimbaji wadogo nao wanaweza kuyaendeleza kwa haraka zaidi.
Naye DC Msangi alisema kuwa amesikia kilio cha wachimbaji hao na kuahidi kulifanyia kazi suala hilo kwa kushirikiana na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo ili kumshawishi mwekezaji wa mgodi huo kuwapatia eneo hilo
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa