Home » » Wakazi walia na maafa ya kila mwaka

Wakazi walia na maafa ya kila mwaka

WANANCHI wa kitongoji cha Mwayunge mjini Igunga mkoani Tabora wameulalamikia uongozi wa wilaya hiyo kwa kushindwa kudhibiti maafa yanayotokea kila mwaka nyakati za masika.
Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti, wananchi hao walisema kuwa maafa hayo yamekuwa yakitokea kila mwaka katika kitongoji chao kutokana na maji kujaa na kukosa mwelekeo.
Wananchi hao walisema kuwa dimbwi lililopo katika kitongoji hicho hujaa maji wakati wa mvua za masika zinapoanza kunyesha na kuingia katika nyumba za watu na kusababisha maafa hayo.
Walisema kuwa ni zaidi ya miaka mitatu maafa hayo yameendelea kujitokeza na kusababisha athari kwa wananchi baada ya nyumba zao kuharibiwa na mvua hizo.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Selemani Saidi, alisema kuwa halmashauri ya wilaya hiyo inatumia gharama kubwa pindi yanapotokea maafa huku wakisahau kuchimba mitaro ili maji hayo yapate mwelekeo na kuepusha maafa hayo.
Naye Mwenyekiti wa Kitongoji, Ally Isike, alisema kuwa halmashauri ya wilaya hiyo imeahidi kuchimba mitaro ya kupitisha maji hayo, lakini hadi sasa bado haijatekelezwa.
Kwa upande wake, mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Rustika Turuka alikiri kuwepo kwa tatizo hilo la maafa kila mwaka na kusema kuwa amejipanga kutatua kero hiyo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa