Home » » PIMENI MAENEO YA SHULE NA KUWEKA MIPAKA ILI WANANCHI WASIENDELEE KUYAVAMIA- NZUNDA

PIMENI MAENEO YA SHULE NA KUWEKA MIPAKA ILI WANANCHI WASIENDELEE KUYAVAMIA- NZUNDA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na Tiganya Vincent
RS-Tabora
21 Novemba 2017
WAKURUGENZI Watendaji wameagiza kuhakikisha maeneo ya Shule na Taasisi nyingine za elimu yanapimwa haraka na kuwekewa mipaka ili kuepuka uvamimizi unaofanywa na watu na kusababisha migogoro ambayo imekuwa ikichelewesha maendeleo.
Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni mkoani Tabora na Naibu Katibu Mkuu (ELIMU) Ofisi ya Rais , Serikali za Mitaa na Tawala za Mikoa( TAMISEMI ) Tixon Nzunda wakati akizungumza na Watendaji  na watumishi wa Mkoa huo.
Alisema kuwa hatua hiyo itasaidia kuondoa migogoro kati ya uongozi wa Shule husika na wavamizi wa maeneo hayo.
Nzunda alisema kuwa migogoro inayotokana na uvamizi wa maeneo ya shule imekuwa ikiathiri maendeleo ya wanafunzi na taaluma kwa sababu uongozi wa shule wakati mwingine umekuwa ukishindwa kupanua miundo mbinu kwa ajili ya utoaji wa elimu kwa wanafunzi.
Alisema kuwa ili kuepuka tatizo hilo kuendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali ya shule ni kwa Wakurugenzi Watendaji kwa kushirikiana na watendaji wengine kama vile watu wa mipango miji kuhakiki maeneo yote yanamilikiwa na Shule na kuwaondoa ambao wameingia.
Aidha Naibu Katibu Mkuu huyo aliwaagiza Wakuu wote wa Shule kuhakikisha kuwa maeneo yao yanapandwa miti mipakani na maeneo mengine ya shule ikiwa ni hatua ya kukabiliana na uvamizi unaofanywa na watu wanaoingia baada ya kuona maeneo hajafanyiwa uendeleza wowote.
Aliongeza kuwa pia wanatakiwa kupanda maeneo ya shule maua ikiwa ni sehemu ya kufanya mazingira yavutie wanafunzi kwenda kujifunza.
Katika hatua nyingine Naibu Katibu Mkuu huyo amewaagiza walimu kuhimiza pia masomo ya michezo na Sanaa  mashuleni ikiwa ni sehemu ya kuwavutia wanafunzi wengi kuhudhuria shuleni.
Alisema kuwa ni vema wakatumia fedha kidogo wanayopata kununulia vifaa vya michezo na Sanaa ili kuwapa fursa wanafunzi kuonyesha vipaji vyao mapema ambavyo vinaweza kuwasaidia katika maisha yao ya baadaye kama vitaandaliwa na kulelewa vizuri toka awali.
Nzunda alisisitiza kuwa michezo na Sanaa ni sekta  ambazo zimesaidia vijana kujiari sehemu mbalimbali duniani , hivyo ni vema walimu wasaidie kuwaandaa wanafunzi ili waweze kushiriki kikamilifu katika eneo hilo.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Tabora Bosco Nduguru alisema kuwa kwa upande wao wameshaanza kuwaondoa wavamizi wa maeneo ya Shule ambapo hivi karibuni waliowaondoa wavamizi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Tabora kwa kuvunja nyumba zilizojengwa katika eneo hilo.
Alisema kuwa wanataraji kuwaondoa wakati wowote waliovamia maeneo mengine ya Shule kama wale wa Shule ya Sekondari MIlambo na kwingineko na kisha kuweka uzio.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited : |
Copyright © 2012. Tabora Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za mikoa